Home KITAIFA DK. BITEKO AAGIZA WIZARA YA MAJI KUHAKIKISHA WANANCHI WANAPATA MAJI SAFI NA...

DK. BITEKO AAGIZA WIZARA YA MAJI KUHAKIKISHA WANANCHI WANAPATA MAJI SAFI NA SALAMA

Google search engine

*ASISITIZA WANANCHI KUTOA MAONI UTUNZAJI WA MAZINGIRA KATIKA DIRA 2050, ATAKA BODI ZA MABONDE YA MAJI,NEMC KUDHIBITI UCHAFUZI WA MAZINGIRA

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dk. Doto Biteko akizungumza  wakati wa Maadhimisho ya Kilele cha Wiki ya Maji Tanzania na Siku ya Maji Duniani yaliyofanyika Mtumba Jijini Dodoma 22 Machi 22, 2024.
Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dk. Doto Biteko akizungumza  wakati wa Maadhimisho ya Kilele cha Wiki ya Maji Tanzania na Siku ya Maji Duniani yaliyofanyika Mtumba Jijini Dodoma 22 Machi 22, 2024.

Na MWANDISHI WETU

-DODOMA

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dk. Doto Biteko ameitaka Wizara ya Maji kuhakikisha watanzania  wanapata huduma ya maji safi na salama ili kuendana na thamani halisi ya miundombinu ya maji iliyojengwa na Serikali kwa gharama kubwa ili kuwapa huduma wananchi kwa ufanisi.

Dkt. Biteko ametoa agizo hilo Jijini Dodoma Machi 22, 2024 wakati akifunga  Maadhimisho ya Wiki ya Maji Tanzania ambayo yameenda pamoja na  Siku ya Maji Duniani.

Ameagiza Wizara na Mamlaka za Maji zijielekeze kwenye ujenzi  wa miradi mikubwa ya kimkakati ikiwemo mabwawa ya kuvuna maji ya mvua katika maeneo yasiyo na vyanzo vya maji vya uhakika na kusisitiza kuwa suala hilo lisisubiri rasilimali fedha ya kutosha bali waanze kutekeleza na rasimali zitaendekea kuja wakati utekelezaji umeshaanza.

Vilevile ametoa wito kwa mwananchi mmoja mmoja, taasisi za Serikali, binafsi, madhehebu ya dini na makundi mengine kuweka miundombinu ya kuvuna maji ya Mvua  kwenye nyumba zao ili kuimarisha upatikanaji wa maji kutokana na mvua zinavyopatikana.

Akizungumzia hifadhi na utunzaji wa mazingira, Dk. Biteko amewataka wananchi wajitokeze kutoa maoni katika mkakati wa hifadhi vyanzo vya maji wakati huu Serikali ikiendelea na utayarishaji wa Dira ya Taifa ya mwaka 2050  ili suala la hifadhi za vyanzo vya maji lipewe kipaumbe kinachostahili.

Aidha ameagiza Bodi za  Maji na Baraza la Taifa la Uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kuongeza jitihada za kudhibiti uchafuzi wa mazingira na hata wawekezaji wanapokuja nchini lazima wazingatie utunzaji wa mazingira ili yasiathirike.

Katika hatua nyingine, Dk. Biteko amezishukuru sekta binafsi na wadau wa Maendeleo kwa ushirikiano wanaoutoa kwa Serikali katika Sekta ya Maji na kuwaasa kuendelea  kukuza ushirikiano ili kuwasambazia wananchi maji kwani bado kuna kazi kubwa ya kuwapelekea wananchi maji.

Kutokana na hali hiyo, ameitaka Wizara ya Maji kusimamia kikamilifu maeneo yote yenye vyanzo vya maji, kujengea uwezo wataalam wake katika kuandaa maandiko ya maji yatakayowezesha kupata fedha zaidi za mabadiliko ya tabianchi zitakazosaidia kupata fedha za utunzaji wa mazingira na pia Sekta zinazohusiana na maji zishirikikine kwa karibu katika usimamizi na si kila mtu kuwa na sheria yake hali inayoleta ukinzani katika utendaji wa kazi.

Kuhusu mpango uliopo wa uhifadhi wa vidakio vya maji ambao gharama yake ya utekelezaji  ni shilingi bilioni 875 ambazo zinapaswa kutoka Sekta mbalimbali, Dk. Biteko ameagiza Wizara ya Maji kutenga fedha kwenye bajeti yake ili kuhakikisha kuwa mpango huo unatekelezeka.

Amesema vyanzo vingi vya maji vimeharibika  na vingine vinaendelea kuvamiwa hivyo Siku ya kilele cha Wiki ya Maji  kila mtu ajitathmini na kuchukua hatua kuhusu juhudi zinazowekwa kwenye utunzaji wa mazingira ili vizazi vinavyokuja vikute mazingira yaliyo salama.

“ Tafiti za maji za mwaka  2019 zinaonesha kuwa, kiasi cha maji kinachopatikana kwa mtu kwa mwaka kinaendelea kupungua siku hadi siku kutoka mita za ujazo 12,600 katika kipindi cha Uhuru hadi mita za ujzo 2,105 kwa mwaka 2022 hivyo tusipochukua hatua na jitihada za makusudi hali hii itaendelea kushuka kila mwaka kwa sababu maji yanaendelea kupungua katika vyanzo,” amesema Dk. Biteko

Dk. Biteko ametoa pongezi kwa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kuwa kinara wa kumtua mwanamke ndoo kichwani kwa kutenga fedha, kutoa maelekezo na kufuatilia utekelezaji wa miradi ya maji nchini.

Awali, Waziri wa Maji, Jumaa Aweso amesema kuwa  miaka ya nyuma Wizara hiyo ilikuwa ya kero na lawama lakini kutoka Rais Dk. Samia Suluhu Hassan aingie madarakani ameibadilisha  na kuendelea kumtua mama ndoo kichwani na pia ametekeleza miradi mingi ambayo huko nyuma ilikwama.

Amesema katika Vijiji 12, 318 tayari vijiji 9,737 vimesambaziwa maji ambapo amewataka wataalam katika Wizara hiyo kutozoea shida za wananchi hivyo popote pale ambapo maji yanahitajika basi wananchi wapate maji ikiwemo kuchimba visima vitakavyowasaidia wananchi kupata maji.

Viongozi mbalimbali waliohudhuria Maadhimisho hayo ni Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule,  Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, Selemani Jafo na Naibu Waziri wa Maji, Maryprisca Mahundi, Katibu Mkuu Wizara ya Maji, Mhandisi  Mwajuma Waziri na Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji,  Nishati na Madini Zanzibar, Joseph Kilangi.

Google search engine

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here