Home KITAIFA TATHIMINI UJENZI WA BARABARA KWA KUTUMIA TEKNOLOJIA YA KISASA YA ‘ECOROADS’ YALETA...

TATHIMINI UJENZI WA BARABARA KWA KUTUMIA TEKNOLOJIA YA KISASA YA ‘ECOROADS’ YALETA MATUMAINI

Google search engine

Na CATHERINE SUNGURA

-CHAMWINO

TEKNOLOJIA ya kisasa ya ujenzi wa barabara kwa kuboresha udongo kabla ya kuweka lami juu  ijulikanayo kama ‘Ecoroads’ imeonesha matumaini katika miezi sita ya majaribio.

Hayo yamesemwa na Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais-TAMISEMI anayeshughulikia  miundombinu  Mhandisi Rogatus Mativila mara baada ya kutembelea Barabara  zilizojengwa na teknolojia hiyo yenye urefu wa Km. 6.95 wilayani Chamwino.

Mhandisi Mativila amesema kwamba lengo kubwa la kutembelea barabara hizo ni kujionea mafanikio ya matumizi ya teknolojia hiyo ambayo pia inajaribiwa katika wilaya mbalimbali nchini na inatekelezwa  na Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA).

“Lengo la kuja kutembelea barabara hii hapa Chamwino ni kuangalia mafanikio ya matumizi ya teknolojia hii ya kisasa ya kuboresha udongo kabla hatujaweka lami juu inayotekelezwa na TARURA,” amesema

Mtivila amesema kuwa teknolojia hiyo pia inafanyiwa majaribio huko Mufindi, Rufiji na maeneo mengine ili kuweza kuitumia sehemu nyingine ambapo inaweza kupunguza gharama na muda wa ujenzi wa barabara.

“Barabara hii iliyojengwa  inaonekana ni imara na pia sehemu nyingine ya Km. 1.3 haijawekwa lami ila udongo uliokuwa pale umechanganywa na kemikali ambayo tunaendelea kufanyia majaribio tuweze kuona  mafanikio yake.

“Tunafanya hivyo ili kuona kabla haujafunika na tabaka la juu inayozuia maji na vitu vingine je! inaweza kudumu kwa muda mrefu na tayari imeshakaa kwa muda wa miezi sita na tumekuta bado ipo imara kwahiyo inatuonesha hii kemikali inayotumika inahimili na malighafi  ni nzuri lakini bado tunaendelea kuiangalia ili tukiona imefanikiwa itatumika kwa kiwango kikubwa kwenye ujenzi wa  barabara zinazosimamiwa na TARURA,” amesema

Wakati huo huo , Mtendaji Mkuu wa TARURA Mhandisi Victor Seff amesema teknolojia hiyo wilayani Chamwino ni sehemu ya majaribio na tayari wameshafanya katika  maeneo mbalimbali ikiwemo barabara ya  Ilazo-Dodoma (Km. 1) Sawaka-Mkonge-Iyegeya-Lulanda-Mufindi (KM. 10.4) na Utete-Kingupila-Rufiji (Km. 32).

“Tangu ujenzi kukamilika hapa Chamwino  tayari imeshapita  zaidi ya miezi sita lakini bado barabara zina hali nzuri  hivyo sasa hivi  tunaendelea na tathimini ya mafanikio ya hii teknolojia yenyewe ili hapo baadae tuje tuishauri serikali  kama teknolojia hiyo iendelee kutumika katika ujenzi na matengenezo ya barabara zetu,” amesema

Amesema lengo la kuwa na hizo teknolojia ni kupunguza gharama, kuwa na muda mfupi wakati wa ujenzi pamoja na utunzaji wa mazingira.

Mhandisi Seff ameongeza kusema kwamba  licha ya gharama kuwa ndogo lakini bado kuna utofauti ukilinganisha na ujenzi wa kawaida  ambapo  faida ya teknolojia hiyo unaiona moja kwa moja katika muda wa utekelezaji kuwa mfupi akitolea  mfano barabara hiyo ya Chamwino ambayo mkataba wake ulikuwa wa mwaka mmoja ila wameweza kujenga na kukamilisha ndani ya miezi sita.

Naye, Fundi wa magari kutoka mtaa wa Mshikamamo Songo Yusufu amesema barabara hizo za sasa ni bora kuliko za mwanzo ambapo ujenzi wa barabara hizo zimerahisisha kufikiwa na wateja wake kwa urahisi kwani awali barabara ilikuwa na vumbi pamoja na mashimo mengi.

Amesema anamshukuru Rais Dk. Samia Suluhu Hassan  kwa kuwajengea barabara hizo kwani mji umeweza kukuwa na huduma muhimu za msingi wameweza kupatiwa ikiwemo maji na hivyo Chamwino kuwa ya kisasa.

Google search engine

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here